Featured

    Featured Posts

CCM Blog: UFAHAMU MGOGORO SUGU WA ARDHI KATI TAIFA LA ISRAEL (UYAHUDI) NA PALESTINA (KANAANI), UNA HISTORIA NDEFU TOKA ENZI ZA MANABII


1.IBRAHIM (ALIISHI MIAKA 1900 BC),  

2. ISAKA & ISMAIL NA 

3. YAKOBO (YACOUB)

Israel ni taifa pekee la kiyahudi Duniani.

Taifa hili linapatikana Mashariki ya bahari ya Mediterrania, ni taifa dogo kwa eneo, likiwa na ukubwa wa kilomita za mraba 20,770. ( Imezidiwa ukubwa wa eneo na Wilaya ya Sikonge nchini Tanzania kwa tofauti ya kilomita za Mraba 7103 ). 


Israel inapakana na nchi za Syria na Lebanon kwa upande wa kaskazini, Jordan na eneo la Palestina la Ukingo wa Magharibi (West bank) kwa upande wa Mashariki na kusini inapakana na Misri na eneo la Palestina la Ukanda wa Gaza ( Gaza strip ).Taifa hili lina idadi ya watu Milion 8,680,000 kwa takwimu za mwaka 2017. 


Idadi ya Wayahudi ni Milioni 6,484,000 sawa na 74.7% (Idadi hii inajumuisha Walowezi wa Kiyahudi wanaoishi ukingo wa Magharibi (West bank) na eneo la Milima ya Golan). Waisrael Waarabu ni Milioni  1,808,000 sawa na  20.8% ya raia wote wa Israel. Idadi ya Wakristo ambao sio Waarabu pamoja na watu wa jamii ya bahai ni 388,000 sawa na 4.5% ya raia wote wa Israel. Lugha rasmi za Taifa la Israel ni Kiebrania (Hebrew) na Kiarabu (Arabic).


Wapalestina ni jamii ya Kiarabu inayopatikana kwa wingi katika ardhi yao inayokaliwa kimabavu na Israel, kwenye ukingo wa Magharibi wa mto Jordan (West bank) na eneo la Ukanda wa Gaza lililowekewa mzingiro na Taifa la Israel. (Besieged Gaza strip). 


Idadi ya watu Wanaoishi katika ardhi ya Palestina ni milioni 4,543,126 kwa takwimu za mwaka 2017 ambapo Wapalestina ni 3,950,926 na Walowezi wa kiyahudi wanaunda idadi ya watu 5,92,200. Eneo la Ukingo wa Magharibi (West bank) lina ukubwa wa kilomita za Mraba 5,860 na Idadi ya Watu milioni 2,747,943 kwa takwimu za mwaka 2017. Eneo lililozingirwa la Gaza (Besieged Gaza strip) lina ukubwa wa kilomita za Mraba 360 na idadi ya watu 1,795,183 kwa takwimu za mwaka 2017. (Ukubwa wa ukanda wa Gaza umetofautiana kidogo na ukubwa wa Wilaya ya Ilala inayopatikana mkoa wa Dar es salaam nchini Tanzania kwa kilomita tano za mraba). Lugha rasmi za Wapalestina ni Kiarabu (Arabic) na Kiebrania(Hebrew).


UZAYUNI (ZIONISM) NA KUTAWANYIKA KWA WAYAHUDI.

Uzayuni (Zionism) ni Itikadi ya taifa la Israel. Mazayuni (Zionists) wanaamini kuwa Uyahudi (Judaism) ni utaifa na pia ni dini. Na kwamba Wayahudi wanastahili kuwa na nchi yao katika ardhi ya mababu zao kama ambavyo Wachina wanavyostahili kuishi China au Wahindi wanavyostahili kuishi India. Itikadi hii ndiyo iliyosababisha Wayahudi kuanza harakati za kurudi tena katika ardhi ya Palestina na kuunda taifa la Israel mnamo mwaka 1948. Na hiki ndicho chanzo cha mgogoro wa sasa kati ya Wapalestina na Waisrael. 


Waisrael wanapozungumzia Historia ya utaifa wao, huanzia kwenye ufalme wa Daudi (David) ambaye ndiye muasisi wa Ufalme wa Israel uliojulikana kama United Monarch mnamo mwaka 1004- 960BC. Baada ya kifo cha Daudi, mwanaye Suleiman (Solomon) alishika hatamu ya uongozi kuanzia mwaka 961-922BC. Baada ya kifo cha mfalme Suleiman mwaka  922BC Makabila kumi ya upande wa Kaskazini yalikataa kuwa chini ya Utawala wa mfalme Rehoboam ambaye alikuwa ni mtoto wa Mfalme Suleiman, hivyo makabila haya yalifanya uasi na kuanzisha ufalme wao walioupa jina la Ufalme wa Israel-Samaria, mji mkuu wa Ufalme huu uliitwa Samaria, baadae walihamishia makao makuu kwenda mji wa Wacaanan wa Sichem ambao kwa sasa unajulikana kama Nablus. Ufalme huu ulisambaratika baada ya kuangukia mikononi mwa dola ya Assyria ( Assyrian Empire) mnamo mwaka 720BC. 


Hali hii ilipelekea kuwepo kwa falme mbili za Kiebrania za upande wa Kaskazini na upande wa kusini ambayo hii ya upande wa kusini ilibaki kuwa chini ya Mfalme Rehoboam ilijulikana kama nchi ya Yuda (Judah), makao yake Makuu yalibaki katika mji wa Jerusalem na baadae yalihamishiwa katika mji wa Hebron. Ufalme huu ulisambaratika baada ya kushindwa vita na kuangukia mikononi mwa mfalme Nebuchadnezzar wa Babeli mnamo mwaka 587BC. 


Mwaka 63BC nchi ya Yuda iliwekwa chini ya uangalizi wa dola ya Kirumi na mwaka wa 6CE iliunganishwa na kuwa jimbo la Warumi. Mnamo kwaka 135CE Wayahudi waliasi na kupelekea vita baina yao na Warumi ambapo walishindwa vibaya, walipoteza uhuru wao na mji wa Jerusalem uligeuzwa kuwa mji wa kipagani.Wayahudi walipigwa marufuku kuishi Jerusalem na Warumi waliibadili jina nchi ya Yuda na kuiita Syria Palestina.


Kusambaratika kwa falme hizi mbili za kiyahudi na kutawaliwa na madola makubwa kuanza Assyria empire, Babylonian empire, Persian Empire (Iran), Greek empire, Roman Empire, Rashidun Caliphate, Ummayad Caliphate, Ayyubid Dynasty, Mamluk Sultanate, Ottoman Empire na British Empire (United Kingdom) kulipelekea Wayahudi kutawanyika katika maeneo mbali mbali Duniani. Kutawanyika huku kuliwagawa Wayahudi kwa majina kutegemea na maeneo waliyotawanyikia. Makundi haya ya Wayahudi ni Ashkenazi (Ashkenazi Jews) kundi hili ni lile lililohamia katikati na Mashariki ya bara la Ulaya. Sephard (Sephardic Jews ) ni kundi lililohamia maeneo ya kusini ya bara la Ulaya na Kaskazini ya Afrika na Mizrahi (Mizrahi Jews) ambao walibaki mashariki ya kati, Asia ya Kusini na Asia ya kati.


JE WAYAHUDI WALIIKUTA ISRAEL IKIWA TUPU BILA WATU?

Ardhi ya Israel (Palestina) ilikuwa na wenyeji ambao ni makabila ya mwanzo kuja kuweka makazi yao katika nchi ya Palestina. Makabila haya yalihamia huko kutoka kusini na Kaskazini mwa Bara Arabu takriban mwaka 3000 BC. Makabila hayo ni  Wayebusi (Jebusites), Waamori (Amorites), Wahiti (Hittites) Wakanaani (Canaanites) na Waperizi(Perizzites). Makabila haya yalikaa katika maeneo tofauti ya nchi hiyo: Wakanaani waliweka makazi yao katika eneo la Gaza na Wayebusi walibuni mji wa Yebus, ambao kwa sasa unajulikana kama mji wa Jerusalem. Wayebusi walipokonywa mji huo na Wayahudi baada ya kutoka Utumwani nchini Misri mwaka 1003BC chini ya utawala wa mfalme Daudi ambaye aliufanya kuwa makao makuu ya ufalme wake.


Ibrahim ambaye uzao wake ndio unaounda jamii ya wana wa Israel alihamia Palestina wakati huo ikiitwa nchi ya Wacaanan mwaka 1900BC akitokea Kusini mwa Iraq katika eneo lilijulikana kama Uru ya Wakaldayo (Ur of Chaldeans). Ibrahim  aliishi kwa amani na jamii za eneo hilo ambapo alizaa watoto wawili Ismail na Issaack. Ismail na Mama yake walihama Canaan na kuweka makazi yao katika mji wa Makka wakati Issack alibaki Caanan na baba yake Mzee Ibrahim na makazi yao yalikuwa katika mji wa Hebron( Halil). Issack alimzaa Jacob (Yakubu) ambaye naye alifanikiwa kuzaa Watoto kumi na mbili.Kutokana na nchi ya Canaan kukumbwa na baa kali la njaa, Jacob ambaye baadae  alibadili jina na kuitwa Israel na watoto zake walihamia Misri.


Wakiwa Misri walizaliana kwa wingi na kuishi kama watumwa kwa muda wa miaka mia nne (400) hadi Mwaka 1190BC waliporudi katika nchi ya Caanan wakiongozwa na Viongozi wao walioitwa Mussa(Moses) na Joshua Nun (Yusha bin Nuun).  Mussa (Mosses) alifariki wakati wakiwa safarini hivyo Joshua ndiye aliyefanikiwa kuwafikisha katika nchi ya Caanan ambapo walifanikiwa kuteka maeneo kadhaa baada ya kuingia kwenye mapigano na wenyeji wao Wacaanan na makabila mengine. Hapo ndipo Joshua alifanikiwa kuanzisha na kuongoza dola ya Wana wa Israel. 


Dola hii haikuweza kudumu muda mrefu kwani Ilisambaratika baada ya kufa Joshua (Yusha bin Nuun) hivyo Wana wa Israel waliangukia kwenye mateso ya Wafilisti ambao ni jamii ya Wacaanan waliokuwa wakielekea upande wa Kaskazini kutokea kwenye miji yao ya pwani ya kusini ambayo ni Gaza, Ekron, Gath, Ashdod, na Ashkelon. Wana wa Israel wakiongozwa na Sauli (ambaye kwa kiarabu anatajwa kwa jina la Twaaluti) walifanikiwa kuwashinda Wafilisti na kuanzisha tena Dola ya Wana wa Israel mnamo mwaka 1025BC.


 Sauli alifariki mwaka 1004BC na hivyo Daudi alishika uongozi na kuwa mfalme wa Dola ya Israel iliyojulikana kama United Monarch. Ni katika utawala wa mfalme Daudi (King David) ndipo dola ya Israel ilipoimarika na kujitanua katika maeneo mengi ikiwa ni pamoja na kuuteka mji wa Jerusalem kutoka mikononi mwa Wayebusi (Jebusites) mnamo mwaka 1003BC. Mfalme Daudi alifariki mwaka 960 na mtoto wake Suleiman ( King Solomon) alishika hatamu ya Uongozi hadi Mwaka 922BC alipofariki. Kufariki kwa Mfalme Suleiman kulipelekea kugawanyika kwa dola Israel (United Monarch) baada ya makabila kumi ya upande wa Kaskazini kukataa kuutambua utawala wa mfalme Rehoboamu ambaye alikuwa mtoto wa Mfalme Suleiman. Hali hii ilipelekea dola hii kuanguka na kutawaliwa na madola mengine makubwa.


Baada ya kipindi kirefu cha wastani wa miaka 1360 ya kutawaliwa na Madola mbali mbali makubwa kama Assyrian empire, Babylonian empire, Persian Empire (Iran), Greek empire     na Roman Empire kilichopelekea Wayahudi wengi kupelekwa utumwani na wengine kutawanyika sehemu mbalimbali huku wakiziacha jamii nyingine zikiendelea kubaki katika eneo hilo la Palestine (Israel) hatimaye Mji wa Jerusalem uliingia mikononi mwa dola ya Kiislam (Rashidun Caliphate) mwaka 638CE baada ya kuwashinda Warumi wakati dola hiyo ya Kiislamu ilipokuwa chini ya uongozi wa Caliph Omar Al Khatwab ambaye alifunga safari kwenda Jerusalem kuchukua funguo za mji kutoka kwa kasisi Sophronius wa dola ya Kirumi. 


Makabidhiano hayo ya mji wa Jerusalem yalifanyika katika kanisa linajulikana kama the Holy Sepulchre (Church of the Holy Sepulchre ), katika makabidhiano hayo ya mji wa Jerusalem, kasisi Sophronius na Caliph Omar Khatwab walisaini mkataba uliojulikana kama OMAR TREAT, mkataba uliotoa hakikisho kwa Wakristo kuishi na kufanya ibada zao bila kubughudhiwa. Mkataba huo ulisomeka hivi: 


"Haya ndiyo ya amani aliyowapa Umar kiongozi wa Waislamu watu wa Jerusalem. Amewapa amani kwa nafsi zao na makanisa yao na misalaba yao, na kuwa hayatakaliwa makanisa yao wala hayatavunjwa, wala hayatapunguzwa kitu katika majenzi yake wala katika nafasi yake, wala hawatalazimishwa kuacha dini yao wala kudhuriwa yeyote katika wao, na ni juu ya watu wa Jerusalem kutoa jizya (tribute) kama wanavyotoa watu wa Madain"


Ni mwaka huo huo ambapo miji mingi ya Palestina (Israel)iliingia katika Dola ya Kiislamu. 

Ikumbukwe kuwa Caliph Omar ndiye alijenga msikiti mdogo kwa ajili ya kufanya ibada katika eneo ambalo Waislamu wanaamini ndipo ulipokuwa Msikiti wa Mbali (Al Aqsa) uliotajwa kwenye Kitabu kitukufu cha Quran, Sura ya Kumi na Saba (Surat Bani Israil). Kwa mujibu wa mafundisho ya dini ya kiislam, ni eneo hili ambalo Mtume Muhammad aliwaongoza manabii katika ibada kabla hajapaa kwenda mbinguni katika kisa maarufu kinachojulikana kama MIRAJI. Baadae msikiti huo uliongezwa ukubwa hadi kufikia muonekano wake wa hivi sasa. Na kwa mujibu wa imani ya kiyahudi, katika eneo hilo ndipo Mfalme Suleiman (King Solomon) alipojenga hekalu la kwanza. Pia wanaamini kuwa ni katika eneo hilo ndipo patakapojengwa hekalu la tatu na la mwisho. Eneo hilo ni sehemu takatifu kuliko zote katika imani ya kiyahudi. 


MSIKITI WA AL AQSA:

Nchi ya Palestine pamoja na nchi za Sham zote zilibakia katika utawala wa Kiislamu (Rashidun Caliphate) kwa muda wa miaka 461. Ni katika kipindi hicho ndipo jamii za eneo hilo la Palestina zilipojifunza lugha ya kiarabu,  kubadili dini na kuingia katika Uislamu. 


Dola ya Kiislamu ya Rashidun ilipokonywa eneo la Palestina (Israel) mwaka 1099CE na Wakristo kutoka Ulaya walipokuja kuzivamia ardhi hizo katika vita ya Msalaba iliyoshuhudia mauaji ya Waislamu elfu sabini (70,000) katika eneo la Msikiti wa Aqsa ( Temple Mount). Watu wa Msalaba (Crusaders) waliikalia ardhi ya Palestina wa muda wa miaka 88 kabla ya kutimuliwa na Majeshi ya Waislamu wa Ayyubid Dynasty chini ya Sultan wa Syria na Misri mwenye asili ya Kikurdi Swalaahud-Diyn Hasan al-Ayyuubiy ambaye aliweza kuirudisha Palestina mikononi mwa Dola ya Kiislamu mwaka 1187CE. Makao makuu ya dola hii ya kiislamu yalikuwa Cairo  nchini Misri kati ya mwaka 1174CE hadi Mwaka 1250CE, baadae makao makuu ya dola hii yalihamishiwa Allepo nchini Syria mnamo mwaka 1250-1260CE.


Mwaka 1250CE dola ya Kiislamu ya Mamluk ilikamata hatamu ya kuiongoza Palestina na eneo lote la Sham (The Levent) kutoka mikononi mwa utawala wa Swalaahudin Al Ayyuubin (Ayyubid Dynasty). Dola hii ya Mamluk ndiyo iliyopigana na kushinda vita dhidi ya wapiganaji shupavu wa jeshi la Mongol tarehe 6 Septemba 1260CE pale walipoivamia na kutaka kuikalia ardhi ya Sham. Ushindi huu wa dola ya Mamluk dhidi ya Wamongol ulikwenda sambamba na safisha safisha ya mabaki ya Wapiganai wa Msalaba (Crusaders) waliokuwa wamebakia katika maeneo ya ardhi ya Sham ( Syria, Jordan na Lebanon).


Baada ya dola ya Mamluk kuishiwa nguvu, hatimaye ardhi ya Palestina na eneo lote la ardhi ya Sham liliangukia Mikononi mwa dola ya Kiislam ya Ottoman (Ottoman empire) mwaka  1516CE. Dola ya Ottoman iliitawala Palestina kwa muda wa miaka 400 hadi ilipoikabidhi mikononi mwa Utawala wa Uingereza (United Kingdom empire) mwishoni mwa vita kuu ya kwanza ya Dunia mwaka 1918CE. (Rejea: kitabu cha The Palestinian Issue kilichoandikwa na Dr. Mohsen M. Saleh)


KUREJEA KWA WAYAHUDI KATIKA NCHI YA PALESTINA NA KUUNDWA KWA TAIFA LA ISRAEL:-

Kutokana na manyanyaso, kuteswa na kubaguliwa kwa Wayahudi waliokimbilia barani Ulaya, hali hii ilipelekea Wayahudi kuanza kufuatilia kwa ukaribu zaidi asili yao. Ni wakati huo katika karne ya 19 ndipo Wasomi wa kiyahudi walipoona umuhimu wa kuwa na taifa lao katika ardhi ya asili ya mababu zao. Mwandishi wa Kiyahudi mzaliwa wa Austria Theodor Herzl alikuwa mtu wa kwanza kupaza sauti kuhusiana suala la utaifa wa kiyahudi (Jewish nationalism) katika harakati za kimataifa mnamo mwaka 1896. 


Herz ambaye alishuhudia unyanyasaji mkubwa wa Wayahudi alishawishika kuamini kuwa Wayahudi hawangeweza kuishi kwa usalama wakiwa nje ya taifa lao. Aliandika Insha (essays) na kuandaa mikutano iliyochochea uhamiaji mkubwa wa Wayahudi kutoka Ulaya kwenda katika ardhi ya Palestine (Israel). Kabla ya harakati za Herz, ni Wayahudi elfu ishirini tu (20,000) waliokuwa wakiishi katika ardhi ya Palestina. Lakini hadi Adolf Hitler anafanikiwa kukamata madaraka idadi ya Wayahudi iliongezeka mara nane. 


Pia harakati za Wayahudi kurudi katika ardhi ya Palestina zilichochewa zaidi na azimio la Balfour (Balfour Declaration) la mwaka 1917, mwishoni mwa vita kuu ya pili ya Dunia ambapo utawala wa Uingereza kupitia Waziri wake wa mambo ya nje Arthur James Balfour ulitangaza kuanzisha Taifa la Wayahudi kwenye ardhi ya Palestina kupitia barua yake aliyoiandika kwenda kwa Lord Rothschild aliyekuwa kiongozi wa Jumuiya ya Kiyahudi ya Uingereza (British Jewish Community).


Waarabu waliona kumiminika kwa Wayahudi kama ni harakati za ukoloni kutoka Ulaya. Pande hizo mbili za Wayahudi na Waarabu ziliingia katika mapigano makali yaliyoshindwa kudhibitiwa na Utawala wa Uingereza katika Palestina. Mwaka 1947 Umoja wa Mataifa ulipiga kura kuigawa ardhi ya Palestina kuwa nchi mbili. Wayahudi ambao idadi yao ilikuwa 650,000   walikubaliana na uamuzi huo na kutangaza rasmi kuunda Taifa la Israel mnamo 14 May 1948 chini ya David Ben Gurion ambaye alikuwa Mkurugenzi mkuu wa Shirika la kizayuni Duniani (World Zionist Organization).


Wapalestina (Waarabu) ambao idadi yao ilikaribia 1,200,000 waliuchukulia uamuzi huo kama muendelezo wa mkakati wa muda mrefu  wa Wayahudi kuwaondoa katika ardhi zao waliukataa mpango huo. Huo ndio ukawa mwanzo wa Mgogoro wa ardhi unaoendelea sasa baina ya Wapalestina na Waisrael. Wanamgambo wa Wapalestina wakisadiwa na  mataifa ya kiarabu ya Misri, Jordan, Iraq na Syria walitangaza vita dhidi ya Israel mnamo tarehe 15 May, 1948.Vita vilimalizika tarehe 10 March 1949 kwa Israel kushinda na kunyakua ardhi zaidi kutoka mikononi mwa Wapalestina ambao wengi wao waliuawa na zaidi ya laki saba (700,000) kulazimishwa kuondoka katika ardhi zao hali iliyopelekea waishi katika makambi ya wakimbizi tatizo ambalo hadi sasa bado halijapata ufumbuzi. 


Ardhi ya Palestina namna inavyokaliwa na

Waisrael kuanzia mwaka 1946 hadi mwaka 2000.


Hadi kufikia mwaka huu 2017 kuna idadi ya Wakimbizi milioni Saba wa Kipalestina sehemu mbali mbali Duniani ambao Israel imewanyima haki ya kurudi katika maeneo yao. Katika vita hiyo Israel iliongeza ukubwa wa ardhi kutoka asilimia 55 hadi 77. Wapalestina walibaki na asilimia 23 tu ya ardhi inayojumuisha eneo la Ukingo wa Magharibi (West bank) na Ukanda wa Gaza (Gaza Strip). Tukio hili linakumbukwa na Wapalestina kama Nakba ( Janga) au catastrophe kwa kiingereza na huko Israel siku ya Nakba husherehekewa kama kumbukumbu ya kuanzishwa kwa Taifa la Israel. 

Maeneo ya Ukingo wa Magharibi na Ukanda wa Gaza yalitekwa na  Israel mwaka 1967 katika vita ya siku sita (Six day war) kati ya Israel na Mataifa ya Kiarabu ya Misri, Lebanon, Jordan na Syria. Israel iliruhusu Walowezi wa Kiyahudi kujenga makazi katika maeneo hayo ambapo makazi hayo yanachuliwa kuwa sio halali na sehemu kubwa ya Jumuiya ya Kimataifa. 


Wapalestina waliendeleza harakati za kujikomboa kwa kuanzisha vyama vya ukombozi vya PLO (Palestine Liberation Organisation) kilichoanzishwa 28 May 1964 chini ya Yasser Arafat, sasa hivi PLO inaongozwa na Mahmoud Abbas (Abuu Mazen). Chama kingine ni HAMAS kilichoanzishwa mwaka 1987 chini ya Ahmed Yasin na Abdel Aziz al Rantiss, kwa sasa Chama hicho kinaongozwa na Ismail Haniya, waziri mkuu wa zamani wa Palestina . Chama cha Hamas kimejizatiti zaidi katika eneo la ukanda wa Gaza wakati chama cha PLO kikiwa na Ushawishi mkubwa katika eneo la ukingo wa Magharibi wa mto Jordan (West bank).


Kutokana na kuimarika kwa harakati za Mashambulizi ya Hamas kupitia tawi lao la kijeshi la Izzudin al Qassam brigades linaloongozwa na makamanda shupavu Mohammed Deif na  Marwan Issa dhidi ya Walowezi wa Kiyahudi huko Gaza, Israel ililazimika kujiondoa Gaza na kubomoa makazi yote ya Walowezi wa Kiyahudi. Hatua hiyo iliipa Hamas hatamu ya uongozi katika Ukanda wa Gaza. 


Hata hivyo tangu Mwaka 2005 Israel kwa kushirikiana na Misri zimeendelea kuiwekea vikwazo Gaza kwa kuiwekea Mzingiro wenye lengo la kuzuia uingizaji wa silaha na harakati za wapiganaji wanaoingia na kutoka kwenye eneo hilo. Mzingiro huo umeleta madhara makubwa kwa wananchi wa Gaza kwa kulifanya eneo hilo kukosa mahitaji mengi muhimu ya kibinadamu kama mafuta, nishati ya umeme, na uagizaji wa  bidhaa za viwandani kutoka nje.  


Kujitoa kwa Israel kutoka ukanda wa Gaza (Unilateral Withdrawal) ilikuwa mwanzo wa taifa hilo la Kiyahudi kuanza harakati kubwa za ujenzi wa makazi ya Walowezi wa kiyahudi katika eneo la ukingo wa magharibi (West bank) ukiwemo mji wa Jerusalem Mashariki ambao Wapalestina wanatarajia kuwa ndio utakaokuwa Mji mkuu wa Taifa lao. Hadi mwaka huu 2017 idadi ya Walowezi wa Kiyahudi katika eneo hilo inafikia laki tano (500,000) ambapo Israel imeshasisitiza kuwa Jerusalem kamwe haitagawanyika na ndio mji wao mkuu wa milele. 


Ukiondoa Marekani ambayo Mwezi Desemba 2017 kupitia Rais Donald Trump imetangaza rasmi kuitambua Jerusalem kama mji mkuu wa Israel na kuagiza Ofisi za ubalozi wa Marekani zihamishiwe Mjini Jerusalem kutoka jijini Tel Aviv, bado jumuiya ya Kimataifa imeendelea kutotambua msimamo huo wa Israel ambapo nchi nyingi zimefungua balozi zao Mjini Tel Aviv.


Eneo la West bank lina kumbukumbu Muhimu sana kwa dini za Kiyahudi, Kiislamu na Kikristo kutokana na kuwa na urithi wa maeneo matakatifu kwa dini hizo kama vile Misikiti ya Al Aqsa (The dome of the rock) na Haram al sharif (Temple mount) inayopatikana mjini Jerusalem, pia kuna Church of the Holy Sepulchre. Maeneo mengine ni Msikiti wa Ibrahim (Cave of the Patriarchs) mjini Hebron na Church of Nativity mjini Bethlehem ambako ndipo inasemekana alizaliwa Yesu Kristo.


JE WAISRAEL WATAENDELEA KUIKALIA ARDHI YA PALESTINA MILELE?

Ni swali linalosumbua sana Wanasiasa wa Israel kutokana na wingi wa makazi ya Walowezi wa kiyahudi kwenye ardhi ya Palestina huko ukingo wa Magharibi. Vyama vya siasa  vya mrengo wa Kushoto, kati na kulia vimekuwa na mitazamo na sera tofauti kuhusiana na hatima ya makazi ya Walowezi wa Kiyahudi katika ardhi ya Palestina.


Misimamo ya vyama vya mrengo wa kulia:

Chama cha Likud chenye Wabunge 30 kati ya Wabunge 120  katika bunge la Israel (Kneset) kinachoongozwa na Waziri mkuu Binyamin Netanyahu, Bayit Yehudi (Jewish Home) chenye wabunge 8 kinachoongozwa na Waziri wa Uchumi Naftali Bennett, United Torah Judaism chenye Wabunge Sita  kinachoongozwa na waziri wa afya Yaakoov Litzman na SHAS chenye wabunge saba kinachoongozwa na Waziri wa Mambo ya ndani Aryeh Deri vinapinga kuanzishwa kwa taifa la Palestina. Vyama hivi vinavyoongoza serikali ya sasa ya Israel vinaunga mkono ujenzi wa makazi ya Walowezi wa kiyahudi kwenye ardhi ya Palestina. 

Msimamo wa vyama hivi ni kuwa na Taifa moja la Israel lenye wakazi wa jamii za Kiyahudi na Kiarabu ambao watakuwa na uhuru wa kuishi sehemu yeyote ndani ya Israel. 


Kwenye kampeni za uchaguzi za mwaka 2015 Waziri Mkuu Binyamin Netanyahu akihutubia katika makazi ya walowezi wa kiyahudi ya Har Homa (Har Homa Settlements) aliahidi kujenga maelfu ya makazi ya walowezi wa kiyahudi kwenye ardhi ya Palestina na kusisitiza kuwa hatoruhusu kuundwa kwa Taifa la Palestina katika utawala wake.


Naftari Bennett mtoto wa Wahamiaji wa kiyahudi kutoka Marekani na Mwanamama Ayelet Shaked (Waziri wa Sheria wa Israel) kutoka chama cha Bayit Yehudi ni wanasiasa wenye misimamo uliyofurutu mipaka wanaotaka Wapalestina wote wachukue uraia wa Israel na wale wasiotaka basi waishi Israel kwa vibali maalum kama raia wa kigeni au wakimbizi. Pia wanapinga haki ya kurejea nyumbani kwa wakimbizi wa Kipalestina waliokimbia wakati wa vita vya mwaka 1948 na 1967.


Chama kingine cha Mrengo wa kulia cha Yisrael Beiteinu (Israel nyumbani kwetu) chenye wabunge 5, kinachoongozwa na Waziri wa ulinzi Avigdor Lieberman kinaunga mkono kuundwa kwa Taifa la Palestina. Chama hicho kupitia mpango wake unaojulikana kama Lieberman Plan (Populated Area Exchange Plan) kinataka Miji yote ya mipakani ya Israel yenye wakazi wengi Waarabu kama vile Umm el Fahm, Tayyibe, Ar'ar, Baqa al-Gharbiyye,Kafri Qara,Qalansawe, Kafr Qasim, Tira, Kafr Bara na Jaljulia ihamishiwe Palestina kwa kubadilishana na Makazi makubwa ya walowezi wa kiyahudi yaliyojengwa kwenye ardhi ya Palestina inayopakana na Israel kama vile Beital Illit, Ma'ale Adumin na Modi'in Illit. Kwa mujibu wa mpango huo Israel itajiondoa katika makazi mengine machache yaliyojengwa maeneo ya ndani zaidi kwenye ardhi ya Palestina.


MSIMAMO WA VYAMA VYA MRENGO WA KATI; Vyama vyote vya mrengo wa kati vinavyounda kundi la Zionist Union vya Hatnua chenye Wabunge watano kinachoongozwa na mwanamama Tzipi Livn, Labor cha Avi Gabbay chenye wabunge 19, Green Movement cha Yael Cohen ambacho kina mbunge mmoja na Yesh Atid chenye wabunge 11 kinachoongozwa na Mwandishi wa habari Yair Lapid, pia chama cha Kulanu cha Moshe Kahlon chenye wabunge 10 vinaunga mkono Israel kujiondoa katika maeneo ya Palestina kupitia mpango wa kuanzishwa kwa mataifa mawili (Two state Solution). Isipokuwa msimamo wao kuhusu hatima ya mji wa Jerusalem hautofautiani na ule wa vyama vya mrengo wa kulia ambao unasisitiza kuwa Jerusalem isiyogawanyika ndio mji mkuu wa milele wa Israel. Pia vyama hivyo vinaunga mkono ujenzi wa ukuta (Separation wall ) utakaotenganisha eneo la Palestina la West bank na Israel.Mpango wa kujenga Ukuta ulianzishwa na Waziri mkuu wa zamani hayati Ariel Sharon lakini haukuweza kukamilishwa hadi sasa. 


MSIMAMO WA VYAMA VYA MREGO WA KUDHOTO;

 Vyama vya mrengo wa kushoto  vinavyounda United Arab Joint List vya Hadash (The Democratic Front for Peace and Equality) chenye wabunge watano kinachoongozwa na Ayman Odeh, Balad (National democratic assembly) chenye wabunge watatu kinachoongozwa na Jamal Zahalka, Ta'al (Arab Movement for Renewal) chenye wabunge wawili kinachoongozwa na Ahmad Tibi, na United Arab List chenye Wabunge watatu kinachoongozwa na Masud Ghnaim vinapinga ujenzi wa Makazi la walowezi kwenye ardhi ya Palestina, pia vinataka kuundwa kwa taifa la Palestina ambalo mji wake mkuu utakuwa Jerusalem Mashariki. Pia msimamo wa chama cha Wayahudi cha Meretz chenye wabunge watano   kinachoongozwa na Zehava Gal-On hautofautoani sana na Msimamo wa vyama vinavyounda United Arab List.


Kutokana na tofauti hizo za kimitazamo baina ya vyama vya siasa vyenye nguvu kuhusu namna ya kutanzua mgogoro wa Palestina na suala la Makazi ya walowezi wa kiyahudi, uhakika wa Walowezi hao kuendelea kuikalia ardhi ya Palestina ni mdogo kwani Wakati wowote wanaweza kuondolewa


kutegemea na sera za chama kilichopo Madarakani na makubaliano yatakayofikiwa baina ya Wapalestina na Waisrael.


NINI SULUHISHO LA KUDUMU LA HUU MGOGORO

Kutokana na sababu za kihistoria, jamii zote mbili za Wayahudi (Waisrael) na Waarabu (Wapalestina) zina haki ya kuishi katika eneo hilo na kumiliki ardhi. Kila upande unapaswa kutambua na kuheshimu haki za upande mwingine. Mgogoro huu unaweza kutatuliwa kwa njia mbili tu ambazoni ni ama kuwa na Taifa moja lenye watu wa jamii mbili zenye kuishi pamoja (One state solution) au kuwa na mataifa mawili ya jamii mbili zinazopakana (Two state Solution) kama ilivyoamuliwa mwaka 1948 na Umoja wa Mataifa. 


Wazo la kuwa na Taifa moja (One state solution):


Halikubaliki miongoni mwa Wapalestina ambao wana hofu kuwa hatua hiyo itawafanya wapoteze utambulisho wao na kufanywa watu wa daraja la pili nchini Israel. Kwa upande wa Israel wazo hili linakubalika zaidi na wanasiasa wa mrengo wa kulia nchini Israel ambao wanataka kuiona Israel ikiwa ni taifa moja. Wasichokitaka wanasiasa hao wa mrengo wa kulia ni haki ya Wakimbizi wa Kipalestina zaidi ya 7000,000 walioko nje ya Israel kuruhusiwa kurejea nchini humo.Hofu yao ni kwamba Waarabu watakuwa wengi (Majority) kuliko Wayahudi hivyo kupoteza hadhi ya Israel kuwa taifa Kiyahudi ( Jewish state ).


Wazo la Kuwa na Mataifa Mawili (Two state solution).


Linakubalika kwa Wananchi na Wanasiasa wengi wa pande zote mbili. Kikwazo kikubwa katika utekelezaji wa mpango huu ni hatma ya mji wa Jerusalem na Makazi (Settlements) ya Walowezi wa kiyahudi yaliyojengwa katika ardhi ambayo Palestina wanatarajia ndio iwe nchi yao. Ikiwa Palestina wataendelea na dai lao ya kutaka Jerusalem Mashariki kuwa mji mkuu, Israel inaweza kumaliza mgogoro kwa kuamua kuitwaa Jerusalem, kuondoa Makazi ya walowezi, kujenga mpaka wa ukuta utakaotenganisha Israel na eneo la Palestina la ukingo wa magharibi na kisha kuondoa wanajeshi wake kutoka ukingo wa Magharibi bila kushauriana na upande wowote (Unilateral Withdrawal). Kwa hatua hii Palestina itakuwa imepoteza dai lake la mji wa Jerusalem huku ikirejesha maeneo mengine yote yaliyokuwa yanakaliwa.


SULUHISHO LINALOKUBALIKA KIMATAIFA


 • Ni Israel kukaa meza moja na nchi za Palestina na Jordan ili kujadili na kufikia makubaliano juu ya hatma ya Wayahudi kufanya Ibada na kuzuru maeneo matakatifu yaliyopo Jerusalem Mashariki. 


 • Kuondoa Makazi (Settlements) yote ya walowezi wa kiyahudi kwenye eneo la Ukingo wa Magharibi.


 • Kujiondoa kijeshi katika ardhi yote ya Palestina kwa kurudisha majeshi yake hadi kwenye mpaka wa Mwaka 1967 kabla ya vita ya siku sita. (1948 Armistice border)


 • Kuondoa mzingiro uliowekwa dhidi ya Wapalestina huko Ukanda wa Gaza. 

Kwa kufanya hivyo Palestina itakuwa huru. Mgogoro wa haki ya Wakimbizi wa Kipalestina kurudi nchini mwao utakuwa umemalizika na nchi hizo mbili zitaweza kuishi pamoja ambapo Jerusalem Magharibi itakuwa mji mkuu wa Israel na Jerusalem Mashariki itabaki kuwa mji mkuu wa Palestine

©MASUDI RUGOMBANA

author

Author Name

Author Description!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

www.CodeNirvana.in

Magazeti Ya Leo

Copyright © Magazeti ya Leo, Habari Leo Tanzania, Mwananchi, Michuzi, mwanaspoti, nipashe, Udaku | Designed By Code Nirvana